Tunafahamu kwamba Siku ya Kimataifa ya Usafiri wa Majini Duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 26 Septemba ambapo hapa Nchini, Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) husimamia maadhimisho hayo chini ya miongozo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri Baharini (IMO). Aidha, Siku ya Kimataifa ya Usafiri wa Anga Duniani huadhimishwa kila mwaka tarehe 07 Disemba na hapa Nchini, Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA) husimamia maadhimisho hayo chini ya miongozo ya Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga Duniani (ICAO).
Hivyo, Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuzingatia misingi ya utawala bora na inayotambua na kuthamini maazimio ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, imeamua kuanzia mwaka 2025 madhimisho haya yafanywe kupitia Wizara ya Uchukuzi na LATRA, kwa jina la Wiki ya Usafiri Endelevu Ardhini 2025 sambamba na Siku ya Usafiri Endelevu Duniani 2025. Kauli Mbiu ya maadhimisho haya ni Nishati Safi na Ubunifu katika Usafirishaji (Green Transport and Innovation). Kauli Mbiu hii inasisitiza jukumu muhimu la mifumo ya usafiri shirikishi, yenye ustahimilivu na iliyo rafiki kwa mazingira katika kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu, na Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi.
Kwa kuzingatia ukweli kwamba ufanisi wa huduma za usafiri wa majini na usafiri wa anga vinategemeana na ufanisi wa usafiri ardhini, TCAA na TASAC ni washiriki katika maadhimisho haya. Aidha, LATRA tumeshirikiana na pacha wetu Mamlaka ya Usafiri na Usalama Barabarani ya Zanzibar (ZARTSA). Taasisi zetu hizi, LATRA, TASAC, TCAA na ZARTSA, zimeshirikiana pia katika maandalizi ya maadhimisho haya, na zote zinashiriki maonesho yanayoendelea Mnazi Mmoja.

