Majukumu ya Mamlaka yameainishwa katika kifungu cha 5(1) cha Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini Sura ya 413 kama ifuatavyo;
(a) Kutekeleza majukumu yaliyoainishwa katika Sheria za kisekta;
(b) Kutoa, kuhuisha na kufuta leseni za usafirishaji;
(c) Kwa kuzingatia masharti ya Sheria za kisekta Mamlaka itafanya yafuatayo —
(i) Kusimamia na kutekeleza viwango vya ubora wa huduma na usalama katika sekta zinazodhibitiwa;
(ii) Kuweka vigezo na masharti vya utoaji wa huduma zinazodhibitiwa; na
(iii) Kudhibiti viwango vya tozo za huduma;
(d) Kusajili wahudumu na kuthibitisha madereva wa vyombo vinavyodhibitiwa na Mamlaka;
(e) Kuthibitisha ubora wa vyombo na miundombinu ya Reli
(f) Kufuatilia na kutathmini utendaji wa sekta zinazodhibitiwa, ikiwemo—
(i) Viwango vya uwekezaji;
(ii) Upatikanaji wa huduma salama, zenye ubora na zinazokidhi viwango vilivyowekwa;
(iii) Gharama za huduma;
(iv) Ufanisi katika utoaji huduma; na
(v) Masuala mengine yanayohusika na Mamlaka;
(g) Kuwezesha utatuzi wa malalamiko na migogoro;
(h) Kuelimisha umma kuhusu masuala yanayohusika na Mamlaka na majukumu yake;
(i) Kufanya mashauriano na Mamlaka, taasisi au vyombo vya udhibiti vinavyotekeleza majukumu yanayofanana na yale ya Mamlaka, ndani ya Tanzania Bara au nje ya Tanzania; na
(j) Kutekeleza majukumu mengine yoyote yatakayokabidhiwa Mamlaka kwa mujibu wa Sheria hii au sheria nyingine yoyote husika.

