Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi MUNGU mwingi wa Rehema kwa kuendelea kutupa uhai, afya na kuibariki Serikali yetu ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Pili, naishukuru sana Menejimenti ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) kwa kunipa heshima ya kuwa Mgeni Rasmi katika hafla hii muhimu ya utoaji wa vyeti kwa madereva wa vyombo vya moto vinavyotoa huduma ya usafiri kibiashara waliofanya mtihani na kuthibitishwa na LATRA pamoja na kuzindua mitaala ya mafunzo ya wahudumu wa vyombo hivyo.
Kwa hakika, leo ni siku muhimu sana katika historia ya Nchi yetu na hususan Sekta ya Uchukuzi na Mdhibiti (LATRA) kwa kuweza kutekeleza kifungu cha 5(1)(e) ya Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini, Sura ya 413 iliyopitishwa na Bunge la Tanzania Mwaka 2019 na Kanuni za Usajili wa Wahudumu na Uthibitishaji wa Madereva ya Mwaka 2020. Historia hii inaandikwa na kundi hili la kwanza la madereva takriban 1,000 waliothibitishwa na Mdhibiti ambapo leo tunawakabidhi vyeti vya kuthibitishwa na Mamlaka. Vyeti hivi vitatambulika kitaifa na kimataifa kwa na hasa kwa Nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC), Soko la Pamoja la Mashariki na Kusini mwa Afrika (COMESA) na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).